Msanii atumia noti kutengeneza ndege za kuchezea watoto
"Aonyesha sanaa zake hadharani kwenye kipindi cha Televisheni"
"Benki Kuu yamuonya vikali
PESA hukosa 
thamani lakini heshima yake hulindwa na kubakia palepale. Pesa 
zinapokosa thamani kiasi cha noti kutumika kuchambia chooni na 
kutengeneza ndege za kuchezea watoto basi hapo tena ni makubwa.
Watu wote walioketi karibu na televisheni zao jijini 
Brasilia mji mkuu wa Brazil hawakuamini macho yao kuona msanii 
aliyebobea kwa kuonesha michezo ya watoto akitumia noti za pesa ya nchi 
yao "Cruzeiro"kutengeneza ndege za kuchezea watoto kisha kuzionesha 
kwenye kipindi cha televisheni ya taifa .
Tukio hilo la aina yake siyo kuwa liliwaacha hoi 
wananchi wa Brazil peke yao, bali hata Gavana wa Benki Kuu ya nchi hiyo 
alichukuwa hatua za kuwasiliana na msanii huyo kwa njia ya simu papo 
hapo.
Silvio Santos ni msanii anayeheshimika sana nchini 
Brazil na aliyejizolea sifa kemkem, amelitangaza jina la Brazil hata nje
 ya mipaka ya nchi hiyo.
 Kwa mantiki hiyo, hakuna aliyetarajia kuwa Santos 
angelifedhehesha nchi yake kiasi hicho. Kwa kuheshimu mchango wa Santos 
katika sanaa nchini humo, Gavana wa fedha alimwambia aache mara moja 
utovu wake wa nidhamu vinginevyo wangelimchukulia hatua kali mara moja.
Lakini Mac. Margolis mwandishi anayeandikia jarida 
mashuhuri Brazil la "Veja Journal", anasema kuwa ‘watu hawa wanamuonea 
Santos tu’
Mwandishi huyo anasema kuwa uchunguzi alioufanya 
kwenye mitaa mbalimbali ya Brasilia hususan maeneo ya madogo, wananchi 
walijawa na ghadhabu kufuatia kushuka sana kwa thamani ya pesa yao na 
sasa hawaithamini tena pesa hiyo inayoitwa "Cruseiro"
alishuhudia walevi kwenye vilabu vya usiku 
vichochoroni wakitumia pesa hiyo kwa kuchambia chooni; akina mama 
wanaouza bidhaa walitumia noti hizo kuwafungia wateja wao bidhaa 
walizonunua na hata watu wengine wakizitumia kufuta vumbi kwenye 
madirisha ya nyumba zao na mbaya zaidi ni wauzaji wa madawa ya kulevya 
aina ya "Cocaine" ambao wanatumia pesa hiyo ya Brazil kufunga madawa 
hayo ya kulevya.
Je, ni kwa nini "Cruzeiro" idharaulike  kiasi hicho? 
Wachunguzi wa mambo kwa karibu huko Brazil wanasema thamani ya pesa ya 
nchi hiyo imeshuka kiasi kwamba ilifika wakati mmoja ambapo pesa ya 
Brazil ingeliweza kushindanishwa thamani yake na pesa ya Jamuhuri ya 
Kidemorasia ya Congo Kinshasa na pesa ya Bosnia peke yake. kiwango cha 
kushuka kwa pesa ya Congo Kinshasa inajulikana kwani katika nchi hiyo 
baada ya kifo cha Hayati Joseph Mobutu Seseseko Kuku wa Zabanga wakazi 
wa kijiji anachotokea cha Gbadolite wamekataa kutumia pesa mpya  ya 
serikali ya sasa badala yake wanatumia ile ile ya wakati wa Mobutu.
Kwenye mtaa mmoja wa mji mkuu wa Brazil wa Brasilia, 
mwanamke muuzaji wa bidhaa ametandaza makaratasi lukuki na sarafu zisizo
 idadi hakika huwezi kutofautisha ipi ni pesa na ipi ni bidhaa.
Kwani noti za "Cruzeiro"zimelaliana kiasi cha kuwekwa katika mafungu mafungu mithili ya nyanya.
Nako vichochoroni unakopita penye mitaa ya miji 
mikubwa ya Brazil kama Rio-de-janeiro na Salam siyo jambo la ajabu kwa 
wakazi wa huko kukutana na noti za "Cruzeiro"zilizotupwa mithili ya 
takataka.
Bei za bidhaa ikiwemo vyakula hupanda maradufu 
karibia kila mwezi nchini humo. Wapo wafanyabiashara ambao sasa wameacha
 kutumia "Cruzeiro"na badala yake wanatumia Dola za Kimarekani na Paundi
 ya Uingereza peke yake.
Mtu anayeenda kununua shati moja dukani huko Brasilia, hana budi kubeba kikapu kizima cha noti. 
Ni katika hali hiyo ndiyo msanii Silvio Santos; 
liwalo na liwe akaamua kuithibitishia serikali yake kuwa ni kwa kiasi 
gani pesa yao ni feki.
 Naye akaona yafaa kutengeneza ndege za watoto tu. 
 
