Tuesday, April 16, 2013

PESA HAINA THAMANI TENA...



Msanii atumia noti kutengeneza ndege za kuchezea watoto

"Aonyesha sanaa zake hadharani kwenye kipindi cha Televisheni"
"Benki Kuu yamuonya vikali

PESA hukosa thamani lakini heshima yake hulindwa na kubakia palepale. Pesa zinapokosa thamani kiasi cha noti kutumika kuchambia chooni na kutengeneza ndege za kuchezea watoto basi hapo tena ni makubwa.
Watu wote walioketi karibu na televisheni zao jijini Brasilia mji mkuu wa Brazil hawakuamini macho yao kuona msanii aliyebobea kwa kuonesha michezo ya watoto akitumia noti za pesa ya nchi yao "Cruzeiro"kutengeneza ndege za kuchezea watoto kisha kuzionesha kwenye kipindi cha televisheni ya taifa .
Tukio hilo la aina yake siyo kuwa liliwaacha hoi wananchi wa Brazil peke yao, bali hata Gavana wa Benki Kuu ya nchi hiyo alichukuwa hatua za kuwasiliana na msanii huyo kwa njia ya simu papo hapo.
Silvio Santos ni msanii anayeheshimika sana nchini Brazil na aliyejizolea sifa kemkem, amelitangaza jina la Brazil hata nje ya mipaka ya nchi hiyo.
Kwa mantiki hiyo, hakuna aliyetarajia kuwa Santos angelifedhehesha nchi yake kiasi hicho. Kwa kuheshimu mchango wa Santos katika sanaa nchini humo, Gavana wa fedha alimwambia aache mara moja utovu wake wa nidhamu vinginevyo wangelimchukulia hatua kali mara moja.
Lakini Mac. Margolis mwandishi anayeandikia jarida mashuhuri Brazil la "Veja Journal", anasema kuwa ‘watu hawa wanamuonea Santos tu’
Mwandishi huyo anasema kuwa uchunguzi alioufanya kwenye mitaa mbalimbali ya Brasilia hususan maeneo ya madogo, wananchi walijawa na ghadhabu kufuatia kushuka sana kwa thamani ya pesa yao na sasa hawaithamini tena pesa hiyo inayoitwa "Cruseiro"
alishuhudia walevi kwenye vilabu vya usiku vichochoroni wakitumia pesa hiyo kwa kuchambia chooni; akina mama wanaouza bidhaa walitumia noti hizo kuwafungia wateja wao bidhaa walizonunua na hata watu wengine wakizitumia kufuta vumbi kwenye madirisha ya nyumba zao na mbaya zaidi ni wauzaji wa madawa ya kulevya aina ya "Cocaine" ambao wanatumia pesa hiyo ya Brazil kufunga madawa hayo ya kulevya.
Je, ni kwa nini "Cruzeiro" idharaulike kiasi hicho? Wachunguzi wa mambo kwa karibu huko Brazil wanasema thamani ya pesa ya nchi hiyo imeshuka kiasi kwamba ilifika wakati mmoja ambapo pesa ya Brazil ingeliweza kushindanishwa thamani yake na pesa ya Jamuhuri ya Kidemorasia ya Congo Kinshasa na pesa ya Bosnia peke yake. kiwango cha kushuka kwa pesa ya Congo Kinshasa inajulikana kwani katika nchi hiyo baada ya kifo cha Hayati Joseph Mobutu Seseseko Kuku wa Zabanga wakazi wa kijiji anachotokea cha Gbadolite wamekataa kutumia pesa mpya ya serikali ya sasa badala yake wanatumia ile ile ya wakati wa Mobutu.
Kwenye mtaa mmoja wa mji mkuu wa Brazil wa Brasilia, mwanamke muuzaji wa bidhaa ametandaza makaratasi lukuki na sarafu zisizo idadi hakika huwezi kutofautisha ipi ni pesa na ipi ni bidhaa.
Kwani noti za "Cruzeiro"zimelaliana kiasi cha kuwekwa katika mafungu mafungu mithili ya nyanya.
Nako vichochoroni unakopita penye mitaa ya miji mikubwa ya Brazil kama Rio-de-janeiro na Salam siyo jambo la ajabu kwa wakazi wa huko kukutana na noti za "Cruzeiro"zilizotupwa mithili ya takataka.
Bei za bidhaa ikiwemo vyakula hupanda maradufu karibia kila mwezi nchini humo. Wapo wafanyabiashara ambao sasa wameacha kutumia "Cruzeiro"na badala yake wanatumia Dola za Kimarekani na Paundi ya Uingereza peke yake.
Mtu anayeenda kununua shati moja dukani huko Brasilia, hana budi kubeba kikapu kizima cha noti.
Ni katika hali hiyo ndiyo msanii Silvio Santos; liwalo na liwe akaamua kuithibitishia serikali yake kuwa ni kwa kiasi gani pesa yao ni feki.
Naye akaona yafaa kutengeneza ndege za watoto tu.